Hii ni Kwaresma
Alhamisi asubuhi tarehe 19.03.2026
Yohana 6:1-14
1 Baada ya hayo Yesu alikwenda zake ng'ambo ya Bahari ya Galilaya, nayo ndiyo ya Tiberia.
2 Na mkutano mkuu wakamfuata, kwa sababu waliziona ishara alizowafanyia wagonjwa.
3 Naye Yesu akakwea mlimani, akaketi huko pamoja na wanafunzi wake.
4 Na Pasaka, sikukuu ya Wayahudi, ilikuwa karibu.
5 Basi Yesu alipoinua macho yake akaona mkutano mkuu wanakuja kwake, alimwambia Filipo, Tununue wapi mikate, ili hawa wapate kula?
6 Na hilo alilinena ili kumjaribu; kwa maana alijua mwenyewe atakalotenda.
7 Filipo akamjibu, Mikate ya dinari mia mbili haiwatoshi, kila mmoja apate kidogo tu.
8 Wanafunzi wake mmojawapo, Andrea, nduguye Simoni Petro, akamwambia,
9 Yupo hapa mtoto, yuna mikate mitano ya shayiri na samaki wawili, lakini hivi ni nini kwa watu wengi kama hawa?
10 Yesu akasema, Waketisheni watu. Na mahali pale palikuwa na majani tele. Basi watu waume wakaketi, wapata elfu tano jumla yao.
11 Basi Yesu akaitwaa ile mikate, akashukuru, akawagawia walioketi; na kadhalika katika wale samaki kwa kadiri walivyotaka.
12 Nao waliposhiba, aliwaambia wanafunzi wake, Kusanyeni vipande vilivyobaki, kisipotee cho chote.
13 Basi wakavikusanya, wakajaza vikapu kumi na viwili, vipande vya mikate mitano ya shayiri vilivyowabakia wale waliokula.
14 Basi watu wale, walipoiona ishara aliyoifanya, walisema, Hakika huyu ni nabii yule ajaye ulimwenguni.
Yesu ni chakula cha uzima;
Asubuhi ya leo tunasoma Yesu akilisha watu 5000, ni kama somo la mahubiri la Jumapili iliyopita, tofauti ni kuwa Jumapili tulisoma Injili ya Mathayo. Yohana haonekani kuandika habari walizoziandika Mathayo, Marko na Luka, anaiandika ishara hii tu (ukiondoa kufufuka kwa Yesu). Sababu mojawapo inaaminika kuwa Yohana aliandika hii ishara kumdhihirisha Yesu Kristo kama chakula cha uzima, yaani neno aliyetoka mbinguni kwa ajili ya wokovu wa wanadamu.
Katika hali ya wanafunzi kutaka watu waondoke, Yesu anaamuru wapewe chakula. Anabariki mikate mitano na samaki wawili, watu wanakula na kusaza. Kwa ishara hii Yesu anaonesha huruma yake, ukarimu wake, lakini uwezo wake kama mwanadamu na Mungu kweli. Kupitia ishara hii Yesu anadhihirisha kwamba yeye ni zaidi ya chakula cha mwili, ni chakula cha uzima, yaani Mwokozi wa Ulimwengu. Mwamini sasa uokolewe. Amina
Alhamisi njema
Heri Buberwa
Mlutheri
