Hii ni Pasaka;
Jumatano asubuhi13.05.2026;
Nehemia 1:1-11
1 Habari za Nehemia, mwana wa Hakalia. Ikawa katika mwezi wa Kisleu, mwaka wa ishirini, nilipokuwapo Shushani ngomeni,
2 Hanani, mmoja wa ndugu zangu, akanijia, yeye na watu wengine waliotoka Yuda; nami nikawauliza habari za Wayahudi waliopona, hao watu wa uhamisho waliosalia; na habari za Yerusalemu.
3 Wakaniambia, Watu wa uhamisho, waliosalia huko katika wilaya ile, wamo katika hali ya dhiki nyingi na mashutumu; tena ukuta wa Yerusalemu umebomolewa, na malango yake yameteketezwa kwa moto.
4 Hata ikawa niliposikia maneno hayo, nikaketi, nikalia, nikaomboleza siku kadha wa kadha; kisha nikafunga, nikaomba mbele za Mungu wa mbinguni;
5 nikasema, Nakusihi, Ee Bwana, Mungu wa mbinguni, Mungu mkuu, mwenye kuogofya, mwenye kutimiza agano lake na rehema zake kwa hao wampendao na kuzishika amri zake;
6 tega sikio lako, macho yako yakafumbuke, upate kuyasikiliza maombi ya mtumishi wako, ninayoomba mbele zako wakati huu, mchana na usiku, kwa ajili ya wana wa Israeli, watumishi wako; hapo ninapoziungama dhambi za wana wa Israeli, tulizozifanya juu yako; naam, mimi na nyumba ya baba yangu tumefanya dhambi.
7 Tumetenda maovu mengi juu yako, wala hatukuzishika amri, wala sheria, wala hukumu, ulizomwamuru Musa, mtumishi wako.
8 Nakuomba, likumbuke neno lile ulilomwamuru Musa, mtumishi wako, ukisema, Mkikosa, nitawatawanya kati ya mataifa;
9 bali mkinirudia mimi, na kuzishika amri zangu na kuzitenda, watu wako waliofukuzwa wajapokuwa katika pande za mwisho za mbingu, hata hivyo nitawakusanya kutoka huko, na kuwaleta mpaka mahali pale nilipopachagua ili kuliweka jina langu hapo.
10 Basi watu hao ni watumishi wako na watu wako, uliowakomboa kwa uweza wako mwingi, na kwa mkono wako hodari.
11 Ee Bwana, nakusihi, litege sikio lako, uyasikilize maombi ya mtumishi wako, na maombi ya watumishi wako, wanaofurahi kulicha jina lako; nakuomba sana; unifanikishe mimi, mtumishi wako, leo, ukanijalie rehema mbele ya mtu huyu. (Maana, nalikuwa mnyweshaji wa mfalme).
Imetupasa kumwomba Mungu siku zote;
Nehemia alipokea habari mbaya za kuta za Yerusalemu kuvunjwa na watu kuwa taabuni. Itikio la Nehemia lilikuwa kufunga, kuomboleza, na maombi ya toba kwa kuomba rehema ya Mungu. Somo linaonesha Nehemia akimsifu Mungu, anaomba toba kwa ajili ya Israeli na familia yake mwenyewe. Anamuomba Mungu kukumbuka ahadi zake kuwakomboa, iwapo wangemrudia. Nehemia baada ya kuomba anajiandaa kuomba ruhusa kwa mfalme kuelekea Yerusalemu kusaidia kuijenga upya.
Tunajifunza nini;
1. Nehemia baada ya kupata habari za kuta za Yerusalemu kuvunjwa, alienda mbele za Mungu kuomba kwa ajili ya watu wake. Yaani alitambua kuwa ni kwa msaada wa Mungu Israeli ingerejea katika hali yake. Kumbe tunakumbushwa kumtegemea Bwana katika njia na kazi zetu wakati wote. Maombi hutuweka karibu na Mungu, maana hutusikia tuombapo na kutupa haja zetu.
2. Nehemia baada ya kuomba anajiandaa kuelekea Yerusalemu kusaidia kuirejesha upya. Aliomba kwanza, sasa alikuwa anaingia kazini. Huyu alijua kuomba lazima kuendane na kutimiza wajibu. Kumbe nasi tuombe, tutafute, tubishe, maana vyote vinaenda kwa pamoja. Amina
Siku njema.
Heri Buberwa
